AL-SHABABU WAONDOLEWA MOGADISHU

kwa kundi hilo linalojihusisha na mtandao wa al-Qaeda, wasema wachambuzi.
  • Wanajeshi wa AMISOM wakilinda eneo la Afgoye. Kuushikilia mji huu muhimu kutoka kwa al-Shabaab ni ushindi mkubwa kwa vikosi vya majeshi ya ushirika. [Mahmoud Mohammed/Sabahi] Wanajeshi wa AMISOM wakilinda eneo la Afgoye. Kuushikilia mji huu muhimu kutoka kwa al-Shabaab ni ushindi mkubwa kwa vikosi vya majeshi ya ushirika. [Mahmoud Mohammed/Sabahi]
Vikosi vya serikali ya Somalia na vile vya Umoja wa Afrika, (AMISOM) vilichukuwa udhibiti wa Afgoye hapo Ijumaa (tarehe 25 Mei) baada ya siku tatu za kampeni ya kijeshi.
"Al-Shabaab wameshindwa vibaya na ushindi huu wa wazi kwa upande wa vikosi vya serikali na vya AMISOM mjini Afgoye ni pigo kubwa kwa kundi hilo; ambalo kamwe haliwezi kupona,” mchambuzi wa mambo ya siasa, kanali mstaafu Osman Aden, aliiambia Sabahi.
Aden alisema kuichukua Afgoye, iliyo umbali wa kilomita 30 kutoka Mogadishu, kutavirahisishia vikosi vya majeshi ya washirika kuilinda barabara kuu kati ya Afgoye na Baidoa. “Itawezesha pia upatikanaji wa misaada ya kibinaadamu kwa wakaazi walio kando ya barabara hiyo muhimu baina ya Afgoye na mji mkuu,” alisema.
Noor Yusif, mchambuzi wa masuala ya siasa na mtaalamu wa harakati za Kiislamu nchini Somalia, alisema: “Mafanikio ya Jeshi la Taifa la Somalia ya kuutoa mji wa Afgoye kutoka mikononi mwa al-Shabaab, kwa msaada wa AMISOM, ni hatua muhimu ya kijeshi, kuchukua ngome ya mwisho ya waasi karibu na Mogadishu.”
Yusif alisema al-Shabaab imedhoofidshwa tangu kuingia majeshi ya Kenya na Ethiopia nchini hapo mwaka jana. “Operesheni za kijeshi za majeshi ya pamoja na ya kieneo zimeudhoofisha uwezo wa kijeshi wa al-Shabaab,” aliiambia Sabahi. “Kuukomboa mji wa Afgoye bila ya upinzani mkubwa ni alama kwamba al-Shabaab inaporomoka na kwamba sasa haina tena uwezo wa kukabiliana na opesheni ya kjeshi dhidi yake.”

Kuziba njia ya usambazaji kwa wapiganaji wa al-Shabaab

Afgoye imekuwa ngome ya al-Shabaab kwa miaka mitatu na mafanikio makubwa kwa vikosi vya AMISOM tangu kuingia kwake Somalia mwaka 2007.
“Mji wa Afgoye ilikuwa ngome madhubuti ya waasi wa Kiislamu kwa sababu upo kwenye barabara muhimu, ikiuunganisha na mji mkuu, Mogadishu na sehemu za magharibi na kusini za Somalia,” alisema mchambuzi wa masuala ya kisiasa Ahmed Omar. “Ilikuwa ni ngome ya pili muhimu kwa al-Shabaab baada ya mji wa Kismayo.”
“Ushindi huu uliopatikana na majeshi ya Somalia na AMISOM mjini Afgoye ni mafanikio makubwa katika mapambano dhidi ya al-Shabaab. Inawakilisha mwanzo wa mwisho wa harakati ya al-Shabaab,” aliiambia Sabahi.
“Kwa kuchukuwa udhibiti wa Afgoye, vikosi vya Umoja wa Afrika na vya serikali sasa vinaweza kuchukua udhibiti kamili wa njia kuu inayounganisha mikoa kusini na magharibi na mji mkuu.” Alisema ushindi huo utawakatia al-Shabaab njia zao za kusambazia vifaa vya kijeshi na mafao wapiganaji wa al-Shabaab.
“Kuichukuwa Afgoye kutoka mikononi mwa waasi kunaelezea kushindwa tena kwa al-Shabaab, ambayo imekuwa ikikabiliwa na shinikizo la kijeshi kutokana na kampeni ya vikosi vya washirika katika maeneo ya kati na kusini,” alisema.

Usalama wa Mogadishu

Wachambuzi wanasema “Operesheni Shabelle Huru" ambayo ilipelekea kuanguka mwa mji wa Afgoye inadhamiria kusaidia kuimarisha usalama mjini Mogadishu, ambao umo kwenye matayarisho ya mkutano wa kwanza wa Bunge la Taifa la Katiba utakaofanyika hivi karibuni.
“Kampeni hii inachangia katika kuuweka salama mji mkuu, Mogadishu, ambao unajitayarisha kwa mkutano wa Bunge la Katiba ambao utaidhinisha katiba mpya na kutayarisha uchaguzi wa Bunge na Rais utakaofanyika tarehe 20 Agosti mwaka huu,” mchambuzi wa masuala ya siasa Abdul Fattah Osman aliiambia Sabahi.
Kudhibiti mji wa Afgoye kutaimarisha usalama karibu na al-Shabaab na kutawanyima wanamgambo hao wa siasa kali fursa ya kufanya mashambulizi dhidi ya Mogadishu kutokea mji wa Afgoye. Hatua hii itaviruhusu pia vikosi vya usalama kuwashinda al-Shabaab na washirika wake wa al-Qaeda nchini Somalia,” aliongeza.

Al-Shabaab wakimbia

Kujiondoa kwa al-Shabaab katika mji wa Afgoye bila ya upinzani mkali kunafuatia mtiririko wa kushindwa kwao, ikiwemo kujitoa katika maeneo yao mjini Mogadishu mwezi Agosti na kuucha kwao mji wa Baidoa mikononi mwa vikosi vya Ethiopia na Somalia hapo mwezi Februari.
Jenerali Abdi Kareem Yusif Dhagabadan, mkuu wa majeshi ya Somalia na kamanda wa operesheni dhidi ya al-Shabaab, aliahidi kuendelea na operesheni za kijeshi.
"Bado hatujakuwa na udhibiti kamili wa Afgoye na tutaendelea kuwawinda waasi hadi tutakapoweza kuwaponda magaidi wote waliokuwa wakaidi,” aliiambia Sabahi. “Operesheni hizi za kijeshi zitasimama baada tu ya kuwamaliza wote.”
"Wanamgambo wana nafasi ya mwisho ya kujisalimisha,” alisema Dhagabadan, akiwataka wapiganaji wa al-Shabaab kujipeleka mwenyewe kwa vikosi vya serikali.
Luteni Jenerali Andrew Guti wa AMISOM aliiambia Sabahi kwamba al-Shabaab inakimbia. “Waasi wanashindwa vita na wanapoteza matumaini,” aliiambia Sabahi. “Wanakimbia na vikosi vya washirika vinapiga hatua kubwa".
“Operesheni hii ilipangwa vyema na hatua zote za tahadhari zilichukuliwa kuepusha maafa kwa raia,” alisema. Kwa kuikamata ngome ya Afgoye, misaada ya kibinadamu inaweza sasa kufikishwa kwa watu 400,000 wanaoishi kwenye eneo hilo, kwani al-Shabaab alikuwa wamepiga marufuku mashirika ya misaada kuyasaidia makundi yaliyoathirika na yaliyo kwenye mazingira magumu.

Al-Shabaab yakataa kushindwa

Al-Shabaab ilisema kwamba iliondoka kwenye mji wa Afgoye kwa makusudi baada ya vikosi vya Umoja wa Afrika kuingia kwenye mji huo na vifaru.
“Mujahidina walitumia mbinu ya kujiondoa kwenye baadhi ya maeneo, lakini hiyo haimaanishi kushindwa,” alisema Abdiaziz Abu Musab, msemaji wa operesheni za kijeshi za al-Shabaab. “Tutaendelea kupigana na bila shaka tutashinda. Vifaru vya AMISOM havitutishi."
Maofisa wa usalama waliiambia Sabahi kwamba taarifa za al-Shabaab si chochote zaidi ya jaribio la kuinua morali ya wapiganaji wao wanaorudi nyuma.
“Baada ya kupoteza mji wa Afgoye, al-Shabaab inajaribu kuinua morali ya wapiganaji wao walioondoka kwenye maeneo yanayoshikiliwa na vikosi vya washirika, na kuelekea maeneo ya vijijini kwenye miji ya kusini,” alisema Mohammed Abdi Qadir, afisa katika Jeshi la Taifa la Somalia.

Huku wakimbizi wa ndani wakikimbia, mashirika ya misaada yaomba walindwe

Misafara mirefu ya magari na mabasi yanayowasafirisha wakimbizi imekuwa ikielekea Mogadishu. Hapo Alhamis na Ijumaa, eneo hilo lilishuhudia misafara mikubwa kutoka Eilasha na ushoroba wa Afgoye, wakitafuta usalama.
Operesheni ya kuikomboa Shabelle imezilazimisha familia kadhaa kuziacha nyumba zao za muda licha ya AMISOM na serikali ya Somalia zimewataka wabakie majumbani mwao.
Kambi ya Afgoye imekuwa makaazi ya muda kwa kiasi ya wakimbizi 400,000 wa ndani ambao waliziacha nyumba zao mjini Mogadishu na maeneo mengine katika miaka iliyopita kukimbia mapigano na ukame.
Fartuun Ahmed aliiambia Sabahi alikimbia na watoto wake wanane kutoka Eilasha. “Hatuwezi kukaa hapa tena kwa sababu mabomu yanatuangukia na sauti za bunduki ziko kila upande,” alisema. “Watu wanaogopa.”
Naibu Mkurugenzi wa Ofisi ya Uratibu wa Masuala ya Kibinaadamu wa Jumuiya ya Nchi za Kiislamu (OIC) nchini Somalia, Dk. Mohammed Noor Jaal, alizionya pande zinazohusika kuwalinda wakimbizi wa ndani wa Ushoroba wa Afgoye.
“Tunamtaka kila mmoja kuchukua hatua za tahadhari kuzuia majeruhi au maafa kwa raia na wakimbizi wa ndani,” aliiambia Sabahi.
Alisema mashirika ya misaada na washirika wa OIC wanafanya kazi ya kupeleka misaada ya kibinaadamu kwa wakimbizi hao waliokimbia mapigano.
Umoja wa Mataifa pia umezitaka pande zote kuruhusu misaada kamili ya kibinaadamu kwa watu wenye uhitaji kwenye Ushoroba wa Afgoye.
“Ambapo tunaendelea kutokuwa na upande wowote wa michakato ya kisiasa na kijeshi, wafanyakazi wa huduma za kibinadamu wanaratibu shughuli za kuhakikisha kuwa msaada wa haraka unapatikana kwa raia walioathirika vibaya na harakati za kijeshi katika ushoroba huo,” alisema Mratibu wa Masuala ya Binaadamu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia, Mark Bowden, hapo Jumanne.
Unaonaje kuhusu makala hii?

Unaonaje kuhusu makala hii? (Jumla ya Kura 36)

Unaonaje kuhusu makala hii?

Maoni ya msomaji

( Sera za kutoa Maoni )
*Inaonesha Maeneo yanayohitaji
Button

Comments

Popular posts from this blog

DC KIZIGO ATOA MAAGIZO KWA KWA MAAFISA ELIMU KUKABILIANA NA UKATILI MASHULENI.

HISTORIA YA MPWAPWA HATARINI KUTOWEKA

KIZIGO AWAPONGEZA RUWASA,AKERWA NA UHARIBIFU WA MAZINGIRA,AWATAJA MADIWANI.